Mwenyekiti wa UWT taifa Mary Chatanda ameonya watu kuacha kutumia siasa kwenye kambi zilizotengwa na Serikali kwa ajili ya waathirika wa mafuriko na badala yake wafike ameneo hayo kwa ajili ya kuwafariji na kuwapatia msaada watu walioathirika wa mafuriko.
Chatanda ameyasema hayo wakati alipofika kutoa pole na kukabidhi msaada kwa waathiriwa wa mafuriko ya Rufiji, akisema watu wanaofika maeneo hayo kutengeneza siasa huku, hawatakiwi kusikilizwa na wanapaswa kupuuzwa kwani Watanzania wana huzuni na taarifa za athari zilizotokana na mafuriko hayo.
Amesema, "unawahutubia wenzako wakati wanamatatizo, hujiulizi wanafikiria ni namna gani wataishi watoto wao hawaendi shule, nguo zimekwenda, chakula hakuna wewe unakuja kuhutubia kitu gani unaeleza kitu gani. Achaneni na watu wanaokuja kupiga siasa huu sio wakati wa Siasa sasa hivi ni wakati wa kuwasaidia wananchi wetu ambao wamepata changamoto."
Misaada iliyokabidhiwa na Chatanda ni pamoja na vifaa na mahitaji ya akinamama na familia zao yenye thamani ya zaidi ya shillingi milioni 76 vilivyogawiwa katika wilaya ya Rufiji na Kibiti, Shuka 470, Vyandarua 400 vyenye mabelo matano, Vijora 500, Unga wa sembe viroba 76, Maharagwe kg 100, Sukari kg 150, nguo mchanganyoko na ndoo kubwa za plastic 380.