Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimewaomba radhi wananchi wa jimbo la Arusha Mjini kwa kitendo cha baadhi ya madiwani wa chama hicho kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Aliyekuwa Naibu Meya wa Chadema, Viola Likindikoki aliomba radhi jana kwenye eneo la Soko Kuu jijini Arusha wakati wa mkutano wa kampeni.
Alisema chama kinaomba radhi kwa kuwa kitendo cha madiwani kuhama kilisababsha taharuki.
Likindikoki alisema madiwani waliohamia CCM walishindwa kuendana na kasi ya mabadiliko kwa kuwa tangu Chadema ilipokuwa ikiongoza Hhalmashauri ya Jiji la Arusha ilikumbana na mikiki mikiki mingi.
Alisema licha ya vyanzo vingi vya mapato kupelekwa serikali kuu madiwani wa Chadema walitatua changamoto za wananchi ikiwa ni pamoja na kuboresha sekta za afya, elimu na huduma nyingine.
Mbunge wa Arusha Mjini aliyemaliza muda wake, Godbless Lema alisema yeye ataendelea kuwa Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini na kwamba anamfahamu vizuri mgombea ubunge kupitia CCM, Mrisho Gambo na ana uhakika atamshinda.