Dar es Salaam. Wakati kampeni za lala salama kwa jimbo la Ukonga zikiendelea, Chadema kimesema kitajitoa kulinda kura za uchaguzi wa jimbo hilo huku kikiwaonya watakaothubutu kupindisha matokeo.
Wakizungumza kwenye kampeni za chama hicho, zinazofanyika eneo la Mongolandege leo Septemba 11, Chadema wamesema baada ya kupiga kura wataendelea kusimamia shughuli nyingine za kuhesabu kura mpaka kitapoeleweka.
Akizungumza kwenye kampeni hizo, Katibu wa Chadema wilaya ya Ilala Gervas Lyienda amesema Chadema watalinda kura na hawatakubali kupokwa ushindi wao.
“Tujitoe tulinde kura zetu dhidi ya hawa watu wa kijani. CCM imekwisha tangu alipoondoka JK wamebakia kutegemea vyombo vya dola kama polisi. Tunasisitiza kama tukishinda wakapindisha matokeo tutapambana kama mbwai iwe mbwai".amesema Liende
Amesema wembe uliotumika kuinyoa ccm katika uchaguzi wa 2015 utumike pia kumnyoa mgombea wa CCM, Mwita Waitara .
Amesema Waitara aliwasaliti wananchi wa Ukonga kwa kukubali kununuliwa na CCM hivyo hastahili kurudi bungeni.
"Tulilala nje kulinda kura lakini sasa amefika bei lazima tumkatae" amesema.