Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Chadema Dk Vincent Mashinji na viongozi wengine wa chama hicho jana walikaa kwa zaidi ya saa moja katika ofisi za Tume ya Taifa ya Uchaguzi(Nec), wakilalamikia hujuma katika uchaguzi mdogo wa Agosti 12.
Dk Mashinji na viongozi hao walipeleka ushahidi wa barua za malalamiko ya hujuma wanazodai kufanyiwa katika uchaguzi huo.
Uchaguzi unaofanyika Agosti 12, 2018, ni wa jimbo la Buyungu, Kigoma na kata 77 baada ya madiwani wengi, kuhama vyama vya upinzani na kuhamia CCM wakidai wanaunga mkono juhudi za Rais John Magufuli.
Aliyekuwa Mbunge wa Buyungu, Kigoma, Kasuku Bilago amefariki dunia Mei mwaka huu.
Dk Mashinji alisema walifika katika ofisi hizo leo Julai 14 saa 4:50 asubuhi na waliamua kuondoka saa 6:45 mchana baada ya kuelezwa kwamba Mkurugenzi wa Uchaguzi, Dk. Athumani Kihamia asingeweza kuonana nao.
“Tulikuwa na barua mbili mkononi kama ushahidi wa nakala za madai tulizotuma kwa mkurugenzi huyo siku tatu zilizopita kuhusu hujuma katika kata tano za halmashauri ya Tunduma,” alisema
Alizitaja kata hizo ni ya Kaloleni, Majengo, Sogea, Mpemba na Mwaka wa Kati.
“Tulifika pale tukiwa na barua zetu mbili, tulitaka kumuonyesha ushahidi wa nakala ya barua hizi ambazo anasema hazitambui, tumefika pale msaidizi wake akatusikiliza na kuchukua taarifa zetu, akampelekea akiwa katika kikao cha menejimenti, tumesubiri baadaye saa moja imepita(Mkurugenzi) anatuma ujumbe kwamba hawezi kuonana na sisi,”alisema Dk Mashinji.