Dar es Salaam. Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Boniface Jacob amesema msimu mpya wa kuwapokea wanachama, viongozi na madiwani waliotimkia vyama mbalimbali ikiwemo CCM, umeanza.
Jacob ambaye pia ni diwani Ubungo ametoa kauli hiyo leo Jumanne Mei 28, 2019 wakati wa mkutano wake na wanahabari uliofanyika katika ofisi za kanda ya Pwani, Magomeni uliokwenda sambamba kumpokea aliyekuwa mjumbe wa Baraza la Kuu la Taifa la Chadema, Gango Kidera aliyetokea CCM.
Meya huyo wa Ubungo amesema msimu huo umeanza baada ya chama hicho kikuu cha upinzani nchini kutoa ruhusa ya waliokuwa wanachama wake kurejea.
"Mwanzoni chama kilikataa lakini sasa hivi kimekubali warejee ndio maana mnamuona Kidera yupo hapa. Huyu ni wa moto ametoa CCM asubuhi na sasa hivi mchana amejiunga na chama chake cha zamani.”
" Siyo huyu wapo wengi akiwamo mmoja aliyekuwa kiongozi wa chama fulani cha upinzani kisha akaamua kujiunga na CCM baada ya kuridhishwa na kazi nzuri ya Rais John Magufuli. Huyu ambaye simtaji ametufuata na kutuomba ushauri baada ya kuona chama chake cha zamani hakieleweki na tukamwambia hatuna tatizo aje, muda ukifika mtamuona," amesema Jacob.
Ameongeza, “Chadema ni kama treni kuna watakaomaliza safari na watakaoshukia njiani lakini kama umeshuka njiani kwa bahati mbaya unaruhusiwa kuchukua Bodaboda na kuikimbiza treni ndivyo alivyofanya huyu.”
Pia Soma
- Daktari hospitali ya wagonjwa wa akili adaiwa kulawiti
- Kesi vigogo TRL yakwama
- Bunge la Tanzania lataka vijiji, vitongoji kutorukwa uunganishaji wa umeme
Kidera amesema ameuamua kurejea Chadema kwa kuwa ndio chama kilichomlea.
“Nimerudi nyumbani nashukuru viongozi wenzangu kwa kunikubalia, naahidi kuwa mtiifu kwa Chadema,” amesema Kidera.