Dar es Salaam. Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amesema chama hicho kitasimamisha wagombea katika ngazi zote kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba, 2020.
Ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Februari 10, 2020 jijini Dar es Salaam katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu ushiriki wa chama hicho katika uchaguzi huo.
Amebainisha kuwa baraza kuu la CUF limeamua kusimamisha wagombea wake nchi nzima kwa nafasi zote ikiwa ni hatua muhimu ya kukijenga chama hicho Tanzania Bara na Zanzibar.
"Chama chetu kitasimamisha wagombea katika nafasi zote nchi nzima. Tutakuwa na mgombea urais wa Tanzania, tutakuwa na mgombea urais wa Zanzibar, tutakuwa na wagombea ubunge wa majimbo yote ya Tanzania Bara na Zanzibar na tutakuwa na wagombea udiwani katika kata zote za Tanzania Bara na Zanzibar," amesema Profesa Lipumba.
Akizungumzia hoja ya vyama vya upinzani kuungana na kusimamisha mgombea mmoja, Profesa Lipumba amesema watakuwa tayari kushirikiana na vyama vyenye nia ya dhati ya kuiondoa CCM madarakani lakini hawatakubali kuungana kwa maslahi ya chama fulani.
"Ushirikiano wenye nia ya dhati utakapokuja tutashirikiana. Tutashirikiana na vyama vyenye nia ya dhati, hatutasubiri mgombea wa CCM atemwe ndipo tuanzishe ushirikiano.”
Pia Soma
- Wagonjwa wa kifafa Tanzania wengi hupelekwa kwa waganga wa kienyeji
- DPP: Watuhumiwa kesi uhujumu uchumi lipeni madeni
- Serikali ya Tanzania yataifisha madini ya Sh42.2 bilioni
- VIDEO: Sumaye ataja sababu kurejea CCM
Mwenyekiti huyo amesema wamefarijika kwa kauli ya Rais John Magufuli aliyewaeleza mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao Tanzania kuwa uchaguzi mkuu wa 2020 utakuwa wa huru na haki.
Lipumba amesema ili jambo hilo kwenda vizuri, amemshauri Rais Magufuli kuondoa zuio la vyama vya siasa kufanya mikutano ya hadhara na akubali kukutana na vyama hivyo ili kumshauri mambo yanayoweza kufanyika kwa muda mfupi, hasa uwepo wa tume huru ya uchaguzi.