Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

CHADEMA yatoa neno maridhiano na Samia

Samia Siasa Mbowe Freeman Mbowe na Rais Samia Suluhu wakiwa Ikulu (Picha ya maktaba)

Fri, 28 Oct 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wenyeviti wa Majimbo Mkoa wa Dar es Salaam wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), wamesema maridhiano yanayofanywa baina ya chama chao na Rais Samia Suluhu Hassan, yatakuwa na matokeo chanya kwa mustakabali wa taifa.

Hayo yalisemwa jana kwa niaba yao na Mwenyekiti wa chama hicho Jimbo la Kawe, Leonard Manyama, wakati wakijibu hoja zilizotolewa na vyama 14 vya upinzani baada ya CHADEMA kutoa msimamo wa ripoti ya kikosi kazi cha kuratibu maoni ya wadau wa demokrasia na vyama vingi.

Baada ya CHADEMA kukosoa ripoti hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili wa Baraza la Vyama vya Siasa, Doyo Hassan, alikishangaa chama hicho kuwa kinapingaje ilhali hawajui kilichoandikwa ndani kwa kuwa bado haijawekwa hadharani.

Akijibu vyama hivyo, Manyama alisema, “Vimesubiri CHADEMA itoe maoni ndipo vijitokeze. Vyama vya namna hii ni vya kuvitazama, kujaribu kuviona havina afya kwa mustakabali wa demokrasia ya nchi.”

Alisema wao wanasimamia alichokisema Katibu Mkuu wao, John Mnyika, na wanaamini maridhiano yanayofanywa na CHADEMA na Rais Samia yatazaa matokeo chanya kwa ajili ya mustakabali wa taifa.

“Katika majimbo yetu tunawaambia wanachama wawe watulivu tukisikia na kusubiri msimamo wa chama chetu katika maridhiano na tutakuwa tayari kutekeleza kile viongozi wetu watatuongoza tufanye.

“Kwa sasa tunasimama na kauli ya chama kwamba taarifa ya kikosi kazi ina mapungufu, ilipaswa kurekebishwa.”

Mwenyekiti Jimbo la Ukonga wa chama hicho, Sweya Rajabu, alisema vyama hivyo vinajitokeza vikiona kuna mshike mshike wa CCM na upinzani.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live