CHADEMA imesema haitashiriki hafla ya kukabidhi taarifa ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 itakayofanyika leo Agosti 21, 2021 Ikulu ya Dar es Salaam na badala yake itaendelea kuweka nguvu zaidi katika ajenda zake za kipaumbele.
Taarifa ya Chadema iliyotolewa na Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na mambo ya nje, John Mrema imesema wamepokea mwaliko kutoka NEC lakini hawatakwenda huku wakitoa sababu tano.
"Tumepokea mwaliko kutoka kwa Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa ajili ya Mwenyekiti wa Taifa, Katibu Mkuu, Mgombea Urais na mgombea umakamu wa Rais kuhudhuria shughuli hafla ya kukabidhi kwa Rais taarifa ya uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020,"
"Chama kupitia barua ya Katibu Mkuu kimemjulisha Mkurugenzi wa Uchaguzi kuwa hatutashiriki hafla iliyopangwa kufanyika Ikulu Agosti 21,"
Chadema ambacho mgombea wake katika nafasi ya urais alishika nafasi ya pili, kimesema hakukuwa na uchaguzi na hawawezi kushiriki tukio lolote linahohalalisha uchaguzi huo, lakini pia kilisema kwa sasa kinaelekeza nguvu zake kuhakikisha mwenyekiti wao na wanachama wanaoshikiliwa na vyombo vya dola wanaachiliwa huru.