TANGA, Muheza: Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga, kimeielekeza serikali mkoani hapa kuhakikisha watumishi wote wanaishi kwenye vituo vyao vya kazi, badala ya kukaa nje ya vituo hivyo, kwani wanawakosesha wananchi kupata huduma bora kwa wakati.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdulrahman wakati wa ziara yake ya kukagua shule shikizi iliyopo katika Kijiji cha Tundauwa, Kata ya Kirare jijini Tanga.
Amesema Ilani ya chama hicho inaelekeza serikali kuhakikisha inasogeza na kutoa huduma bora kwa wananchi wote,hivyo ni wajibu wa watumishi kuishi katika maeneo ya karibu na vituo vyao vya kazi.
"Naielekeza Serikali ya Mkoa wa Tanga kuhakikisha watumishi wote ambao wanaoishi nje ya vituo vyao vya kazi kuhamia kwenye vituo vyao, ili wananchi waweze kupata huduma bora kwa wakati bila ya usumbufu,"amesema Mwenyekiti huyo.
Amesema kwa Mmkoa wa Tanga ni muhimu Kila mtumishi aweze kuishi karibu na kituo chake cha kazi, ili kuongeza ufanisi na kuokoa rasilimali zilizopo kutumika vibaya.