Arusha. Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha kimeibuka na ushindi wa asilimia 100 katika uchaguzi wa Serikali za mitaa uliofanyika Novemba 27, 2019.
Katika uchaguzi huo vyama vya upinzani vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi, ACT- Wazalendo na NLD havikushiriki jambo linalodaiwa kutoa mwanya kwa CCM kuibuka na ushindi.
Mkoa wa Arusha una mitaa154, vijiji 390 na vitongoji 1,505.
Akizungumza leo Jumatano Novemba 27, 2019 katika kikao cha kamati ya ushauri ya Mkoa katibu tawala mkoani humo, Richard Kwitega amesema kati ya halmashauri saba, Halmashauri za Monduli, Longido, Ngorongoro na Arusha DC wagombea wote walipita bila kupingwa.
Amesema Halmashauri zilizofanya uchaguzi ni Jiji la Arusha, katika vituo 15, Halmashauri ya Meru kwenye vituo15 na Halmashauri vya Karatu vituo 26.
"Mafanikio ya uchaguzi huu yametokana na ushirikiano mzuri baina ya wasimamizi wa uchaguzi na viongozi wa ngazi mbalimbali,” amesema.
Akifungua Mkutano huo kaimu mkuu wa Mkoa wa Arusha, Idd Kimanta alipongeza ushirikiano uliopo sasa mkoani humo kati ya vyama vya siasa na watendaji wa Serikali.