Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesema katika miaka 45 tangu kuzaliwa kwake, kimewaunganisha wananchi, kimeimarisha umoja na kuunda mtandao wa uendeshaji wa siasa kwa uwazi, ushirikiano na uhakika.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka alisema hayo jana wakati akiweka jiwe la msingi la ofisi ya CCM Wilaya ya Musoma Vijijini, mkoani Mara.
"Ni jambo la kujivunia kuwa na taasisi yenye mizizi mirefu ya kisiasa, chama kinachojiendesha kimfumo, kimaadili, kinidhamu na hata kutoa maamuzi mazito kwa mujibu wa katiba yake kanuni, miiko na taratibu zake," alisema Shaka.
CCM ilizaliwa Februari 5, mwaka 1977 baada ya kuunganishwa kwa vyama vya TANU na ASP.
Shaka alisema kuunganishwa kwa vyama vya TANU na ASP, kulitengeneza uimara na heshima kwa nchi na CCM.
"Tunawapa heko waasisi wetu kwa uamuzi wa kuziunganisha Tanganyika na Zanzibar baadae TANU na ASP kuungana mwaka 1977. Kwa kweli lilikuwa pigo takatifu dhidi ya maadui wa kisiasa.
Waasisi wetu kimsingi walitafakari kwa kina hadi kupitisha misimamo thabiti kwa maslahi ya taifa," alisema.
Shaka alisema uamuzi wa kuunganisha vyama TANU na ASP,kuliiongezea CCM nguvu za kisiasa na kiuchumi, kuimarika utulivu wa ndani, kuongezeka mitaji, rasilimali watu na vyanzo vya mapato.
Alisema hatua ya kuunganisha vyama si tu ilikuwa ya kizalendo, pia ilifanikiwa kuzima ndoto za wasaka madaraka na kudhibiti wanasiasa wakorofi.
Shaka pia alisema muungano wa Zanzibar na Tanzania Bara ni uamuzi wa kupongezwa uliofanywa na waasisi wa Taifa.