Dar es Salaam. Siku moja baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kutoa taarifa kuhusu uchaguzi mdogo utakaofanyika Juni 17, 2019 na wagombea 29 kati ya 32 kupita bila kupingwa, Chama cha Mapinduzi (CCM) kimesema hali hiyo inaonyesha wapinzani wanaridhishwa na utendaji wake.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi Juni 6, 2019 kuhusu wagombea 29 kupita bila kupingwa, Katibu wa NEC Siasa na Uhusiano wa Kimataifa wa CCM, Kanali Ngemela Lubinga alisema kitendo cha wagombea wa chama hicho kupita bila kupingwa huenda inaashiria wapinzani wanaridhishwa na utendaji wa chama hicho katika maeneo yao.
“Wananchi wanapewa nafasi ya kuchagua kiongozi wanayemtaka bila kujali vyama lakini kama upinzani wameona aliyechukua fomu wa CCM anatosha ni sawa.”
“Hii inaweza kutokana na kuwa vyama vingi vya upinzani bado havijakomaa na wameridhika na utendaji wa CCM kwa kuwa imeshakomaa na imejiimarisha hivyo wanaona hakuna haja ya kuweka mgombea,” amesema Lubinga
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Chama cha Umma (Chaumma), Hashim Rungwe amesema hali hiyo inasababishwa na watu kuchoshwa na chaguzi zenye hila na ndiyo sababu wameamua kuacha kushiriki kwa kuwa hakuna jipya watakalolipata.
Amesema kwa sasa Tanzania hakuna mazingira mazuri ya uchaguzi huku akieleza mfumo mzima umegubikwa na hila na upendeleo kwa chama kimoja huku nguvu kubwa ikitumika kuhakikisha chama hicho kinashinda.
Pia Soma
- Lukuvi awaita Dodoma wadaiwa kodi za pango, ni mashirika na taasisi 270
- Mawaziri wa Nishati EAC kukutana Arusha, timu za maandalizi zaanza kuteta
- Imarisha maelewano na wafanyakazi wenzako kwa njia hii
- Rais Museveni ‘amu-unfollow’ Jose Chameleone kwenye twitter baada ya kujiunga na siasa
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Anna Henga amesema mwendelezo wa watu kupita bila kupingwa ni ishara hasi kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa Oktoba 2019 na uchaguzi mkuu 2020.