Dar es Salaam. Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole ameitaja siri ya ushindi wa chama hicho kwenye uchaguzi mdogo wa majimbo mawili ya Ukonga na Monduli na kata zote 23 kuwa unatokana na kazi aliyofanywa na inayoendelea kufanywa na Rais John Magufuli.
Polepole amesema hayo leo Septemba 18,2018 alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisi ndogo ya CCM Lumumba Jijini Dar es Salaam.
Kauli ya Polepole imekuja kufuatia kumalizika kwa uchaguzi mdogo wa majimbo ya Monduli na Ukonga ambapo CCM imeshinda majimbo yote.
Amesema mambo yote anayofanya Rais ikiwamo ujenzi wa barabara, upatikanaji wa maji, upatikanaji wa umeme watu wanaona.
"Tunashukuru tumepokea uaminifu wao kwetu hii umetokana na kuona kila tunachokifanya," amesema Polepole.
Polepole amefafanua kuwa wametoa maelekezo kama chama mawaziri wote, sekta zote waende wakatie kero za wananchi.
Amesema wanatakiwa kuonekana walipo watu wakatatue kero zao.
"Hatutaki watu wakae maofisini kwa sababu siyo sehemu pekee wanapoweza kutatua kero, yote haya watu wanaona," amesema Polepole.