Dar es Salaam. Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole amesema mwaka huu wataanza kutoa mafunzo ya ufundi bure.
Amesema wanatumia fedha za walipa kodi na za CCM na wamefanya majaribio Kilimanjaro na kuna vijana tayari wana karakana zao.
Polepole amesema hayo leo Septemba 18,2018 alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kwenye ofisi ndogo ya CCM Lumumba jijini Dar es Salaam.
Amesema watatoa elimu hiyo ya ufundi kwa vijana wenye umri kuanzia miaka 18 hadi 35 ambao wamemaliza darasa la saba na kidato cha nne.
“Kama umemaliza darasa la saba, kidato cha nne au cha sita na hutaki kuendelea na mfumo rasmi a elimu, CCM itakusomesha bure kwenye vyuo vya mafunzo na ufundi stadi (Veta) na majaribio yamefanyika Moshi, ”amesema Polepole.
Amesema elimu hiyo ya bure haitolewa kwa chuo kimoja, bali inatolewa kuanzia darasa la kwanza hadi la saba na kidato cha kwanza hadi cha nne.
Polepole amesema wamekusanya fedha nyingi mno na wameanza kwa majaribio mkoani Kilimanjaro.
“Huu ni mpango mkubwa wa Serikali wa kutoa mafunzo ya ufundi stadi mwaka huu,”amesema Polepole.