Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

CCM yaahidi kukamilisha miradi ya maendeleo

CCM Zanzibar (600 X 420) CCM yaahidi kukamilisha miradi ya maendeleo

Tue, 25 Jan 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo amewahakikishia wanachama wa chama hicho na wananchi kwa ujumla kuwa chama hicho kimejipanga kuhakikisha kila kilichoahidiwa katika Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2020-2025, kitatekelezwa kwa kiwango chenye tija.

Alisema hayo jana alipokuwa akizungumza na wananchi na wanachama wa CCM katika maeneo tofauti ya wilaya za Wete na Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba ambako yupo katika ziara maalumu ya siku mbili akiambatana na wajumbe wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa.

“Niwahakikishie Chama Cha Mapinduzi kimejipanga, kitafanya kila linalowezekana kuhakikisha Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020- 2025 ambayo imeahidi mambo mbalimbali ikiwamo maji, umeme, barabara, miundombinu ya elimu, imeahidi mambo mengi ndani yake, inatekelezwa kwa kiwango chenye tija,” alisema na kuongeza: “Ndiyo maana mnaona tunapita kama hivi. Kazi yetu sisi ni kupita kuangalia maendeleo ya utekelezaji wa tulichokiahidi kwenu na ndio kazi tunayoifanya sasa hapa Pemba kwa siku mbili.” Alisema hayo alipokuwa akizungumza na wanachama na wananchi wa Kijiji cha Taifu baada ya kuweka jiwe la msingi kuzindua mradi wa maji katika eneo hilo.

Aidha, Katibu Mkuu huyo wa CCM alitoa salamu na ujumbe wa viongozi wakuu wa serikali, Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi kwa wananchi wa Wilaya ya Wete.

“Rais Samia ameniambia niwahakikishie kuwa ataendelea kushirikiana na Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi kupambana kwa ajili ya miradi na changamoto zinazowakabili ili ndani ya miaka mitano Wilaya ya Wete na Pemba kwa ujumla kuwe na mabadiliko makubwa ya maendeleo,” alisema.

Aidha, Chongolo alisema Rais Mwinyi amemtuma salamu zake kwao, awaeleze wananchi kuwa anajua changamoto ya maji inayowakabili wananchi wa baadhi ya maeneo ya Wete na anawahakikishia maji yatawafikia wananchi wote kama ilivyoahidiwa katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020 - 2025 kama ilivyo kwa Kijiji cha Taifu kilichokuwa na uhaba wa maji kwa zaidi ya miaka 14 na sasa maji yanapatikana ya kutosha.

Aliwataka wananchi kuwa macho kupita na kukagua miradi ya ujenzi wa hospitali za wilaya unaoendelea katika wilaya zote za Kaskazini Pemba ikiwamo Wete ambako zaidi ya Sh bilioni nne zimeshapelekwa na ujenzi unaendelea.

Akizungumza na wanachama na wananchi kwenye Mkutano wa Shina Namba Moja, Tawi la Kiuyu, Kigongoni, Wilaya ya Wete, alitoa wito kwa wana CCM wanaotaka kugombea katika uchaguzi wa ndani mwaka huu wajipime na wajue wajibu wa uongozi ndani na nje ya chama na wasisukumwe na tamaa binafsi bali kutumikia watu.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live