CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema hakina wasiwasi na ushindi wake kwa kuwa kimeweka wagombea wenye sifa na uwezo unaokubalika kwa nafasi zote za urais, ubunge na udiwani.
Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally alisema hayo akiwa Makunduchi katika Mkoa wa Kusini Unguja alipozungumza na wanachama na wafuasi wa chama hicho katika mkutano wa kampeni ulihudhuriwa na mgombea wa chama hicho kwa tiketi ya urais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi.
“Nataka niwajulishe wapinzani kwamba takwimu zinaonesha Chama Cha Mapinduzi kitashinda kwa kishindo kupitia wagombea wetu,” alisema.
Aliwataka wanachama na wafuasi wa chama hicho kuendelea kulinda amani na utulivu huku wakijiepuka kulipiza kisasi kutokana na matukio ya hujuma yanayofanywa yakiwamo mauaji dhidi ya viongozi na wanachama wao.
Mintarafu matukio yaliyojitokeza huko Pemba pamoja na mkoani Njombe ambako Kiongozi wa Umoja wa Vijana (UVCCM) aliuawa hivi karibuni, Dk Bashiru alisema chama kimeliachia Jeshi la Polisi kutimiza wajibu wake ukiwamo uchunguzi wa kina.
“Vijana wetu na wanachama tulieni na msikubali kulipiza kisasi,” alisema.
Dk Bashiru aliwataka wanachama na wafuasi kujitokeza kwa wingi leo kumsikiliza mgombea wa urais wa Tanzania, Rais Magufuli akitangaza sera na ilani ya chama na kumnadi Dk Mwinyi, wagombea wabunge na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa tiketi ya CCM.