Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

CCM Kilimanjaro yaonya makada wanaosaka uongozi

E9091c55f5fa5859e7d15193236dbb78 CCM Kilimanjaro yaonya makada wanaosaka uongozi

Thu, 22 Jul 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Kilimanjaro kimetoa onyo kwa makada wake ambao wanadhoofisha shughuli za chama na utekelezaji wa Ilani kwa kuanza kutafuta uongozi ndani ya chama mwakani kinyume na kanuni.

Katika hatua nyingine, madiwani wa viti maalum wa chama hicho katika Manispaa ya Moshi, wameazimia kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kupokea kijiti cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na siku 100 za utawala wake bora.

Mwenyekiti wa CCM mkoani hapa, Patrick Boisafi alisema hayo wakati akifungua semina ya siku moja ya viongozi wa jumuiya za chama hicho ngazi za shina, mitaa, kata na wilaya.

Makada hao wanadaiwa kuanza kampeni za uchaguzi mkuu wa serikali za mitaa mwaka 2024 na uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Katika semina hiyo iliyoandaliwa na madiwani wa viti maalum manispaa hiyo, Boisafi alisema chama hakitasita kuchukua hatua za kinidhamu kwa makada hao kupitia vikao halali vya chama.

"Nitoe angalizo kwa wanachama walioanza kupita huko mitaani kuwatafutia wagombea wao nafasi za uongozi, tukikubaini tutakuita na sina uhakika kama utatoka salama, tuache waliopo madarakani wamalize kazi waliyopewa," alisema.

Mwenyekiti wa Madiwani wa Viti Maalum, Faidha Hemed alisema wametoa viti mwendo vitatu kwa ajili ya kuwasaidia wenye mahitaji kama njia ya kulikomboa kundi hilo.

Alisema madiwani wa viti maalum wataendeleza ushirikiano na viongozi wengine katika kutekeleza ilani na kuiondolea jamii changamoto mbalimbali ikiwamo katika elimu, afya na ujasiriamali.

Katibu wa madiwani hao, Consolata Lyimo alisema mafunzo hayo yanatokana na ziara za madiwani katika baadhi ya kata na kubaini wanawake wana uhitaji wa elimu ya ujasiriamali, mirathi na malezi bora ya familia.

Chanzo: www.habarileo.co.tz