KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Daniel Chongolo amesema ni lazima Chama kishikane mashati na serikali ili kutimiza kila kilichoahidi wananchi katika Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020-2025.
Chongolo ametoa kauli hiyo wakati akiongea na wananchi wa kata ya Simbo Wilaya ya Igunga Mkoani Tabora alipofika kufanya ziara ya siku mbili kukagua utekelezaji wa ilani na kuhimiza uhai wa chama ngazi ya mashina.
“Sisi tulichoahidi hatuko tayari kuwa waongo, ni lazimi tushikane mashati kutimiza kile ambacho tuliahiadi na hiyo ni kazi ya CCM na Mwenyekiti wa CCM Rais Samia Suluhu Hassan amenituma kufanya kazi hiyo hapa,” amesema.
Chongoloa amesema hayo baada ya kupata malalamiko kutoka kwa Mbunge wa jimbo la Manonga mkoani Tabora Seif Gulamali akiilaumu serikali kutojenga barabara ya Ndala-Simbo-Nkinga-Ziba mpaka Shinyanga vijijini, kwa muda mrefu huku waziri wa ujenzi akiwaambia kuwa atafikiria endapo hiyo barabara itajengwa.