KATIBU wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Geita, Rahel Ndegereki amesema Rais John Magufuli hakuwa na ubaguzi wa jinsi kwenye uteuzi na alimpa mtu fursa ysa kuwa kiongozi kwa kuzingatia uwezo.
Ndegereki alisema kwa kuzingatia hilo Magufuli alifanya uteuzi kwa kuzingatia vigezo na ndio maana wakati wa uongozi wake wanawake wenye uwezo katika nyanja ya uongozi wote walipata fursa kuongoza.
Alisema ukiacha uongozi pia wajasiriamali wanawake wataendelea kumkumbuka Magufuli kupitia vitambulisho vya wajasiriamali ambavyo vimekuwa na mchango mkubwa kwa akina mama katika biashara zao.
Ndegereki alisema jana kuwa, ameshuhudia namna akina mama walivyopiga hatua kimaendeleo ndani ya miaka mitano na hiyo ni ishara kwamba walizipata na kuzitumia fursa za kiuchumi.
Alisema, akina mama ndani ya CCM wataendela kumkumbuka Magufuli kwa mema aliyowafanyia na akawaomba waendelee kujituma katika uzalishaji mali ili kuendeleza azima ya Rais Magufuli kuinua Watanzania kiuchumi.
Katibu wa Umoja wa Wanawake (UWT) Wilaya ya Chato, Neema Mkila alisema kiongozi huyo amekuwa na msaada mkubwa kwao hasa baada ya kuweka msisitizo wa asilimia 10 ya mapato ya halmashauri itolewe mkopo kwa akina mama, vijana na wenye ulemavu.