Dar es Salaam. Katibu wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Zakaria Mwansasu amesema wanachama wa chama hicho watakaochaguliwa kuwania uongozi katika uchaguzi Serikali za mitaa kwa rushwa hawatateuliwa.
Uchaguzi wa Serikali za mitaa unafanyika Novemba 24, 2019 na kwa sasa vyama mbalimbali vya siasa vipo katika hatua ya kwanza ya uteuzi wa wagombea.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumanne Oktoba 22, 2019 Mwansasu amesema uamuzi huo ni mwanzo wa kuanza kuyafanyia kazi maagizo ya katibu mkuu wa chama hicho, Dk Bashiru Ally.
Dk Bashiru ameagiza kurudiwa uchaguzi wa ndani wa kupata wagombea wa CCM katika maeneo yenye malalamiko.
Katika maelezo yake Mwansasu amesema kinachofanyika sasa ni kupitia malalamiko yaliyowasilishwa.
“Kwa sasa tunapitia malalamiko yote yaliyowasilishwa na wanachama walioomba kuteuliwa kuiwakilisha CCM. Baada ya maagizo tunaendelea kushughulikia, kufuatilia na kutekeleza kile alichoagiza.”
Habari zinazohusiana na hii
“Uchaguzi wa ndani ya CCM sio wa ushindani ni kura za maoni kwa hiyo mtu awe ameongoza, wa pili au watatu kama atabainika kura alizopata ni kwa hila au rushwa hatafikiriwa katika uteuzi,” amesema.
Amebainisha kuwa wanachama wa chama hicho tawala nchini Tanzania wamepata mwamko wa kugombea na kupiga kura za ndani kuwapata wagombea wake wa uchaguzi huo.