Dodoma. Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally Machi 23 anatarajiwa kuzindua mkakati wa kukomaza demokrasia katika mashina ya chama hicho jijini Dodoma, lengo likiwa ni kuongeza uwajibikaji wa viongozi na wanachama.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini hapa, katibu wa CCM mkoa wa Dodoma, Jamila Yusuph amesema mkakati huo pamoja na mambo mengine una lengo la kuwawezesha viongozi na watendaji wa chama, hasa ngazi ya mashina kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa kushughulikia kero na changamoto za wananchi.
Amesema mkakati huo unazinduliwa sasa baada kufanyiwa kazi changamoto zilizojitokeza kipindi cha nyuma kutokana na mabadiliko ya mfumo na muundo wa uongozi wa mashina na matawi ya chama hicho.
“Neno demokrasia lina maana pana, kama mkoa dhumuni letu ni kuimarisha misingi ya uongozi bora, uwajibikaji wa viongozi na wanachama pamoja na kuongeza kiwango cha ushiriki wa wanachama katika shughuli za maendeleo. Ndio maana tumeamua kuwa na mkakati wa kukomaza demokrasia.”
“Tukumbuke kuwa mkoa wa Dodoma una mashina 12,510 na matawi 1,234, baada ya uzinduzi huo kama mkoa tutauendeleza kwenye mashina yote,” amesema.
Jamila amesema katika uzinduzi huo, Dk Bashiru atagawa kanuni na katiba za chama hicho sambamba na bendera na Ilani.