Iringa. Katibu Mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally amesema chama hicho tawala kimefungua milango ya kuwasamehe wanachama wake wasaliti, na kueleza taratibu wanazotakiwa kufuata.
Dk Bashiru ametoa kauli hiyo leo Jumanne Novemba 27, 2018 mjini Iringa wakati akizungumza na wanachama wa chama hicho.
“Napenda kutumia hadhara hii kuwaeleza wote ambao waliadhibiwa kwa namna moja au nyingine kwa sababu ya kosa au dhambi ya usaliti, wana nafasi ya kusikilizwa,” amesema.
“Kuna nafasi ya kusamehewa kwa hiyo mfuate taratibu za chama maana zipo wazi kanuni na katiba zetu. Viongozi wenye dhamana kama watakuwa tayari kujitokeza na kuomba msamaha ni jambo liko wazi,” amesema Dk Bashiru.
“CCM ni chama cha wananchi, chama cha binadamu hakiwezi kuendekeza visasi na hakuna sababu ya visasi maana sisi pia tunakosoa na hakuna aliyekamilika.”
Amewataka viongozi wa chama hicho kuanzia ngazi ya chini hadi Taifa wanaodhani sasa wamejirekebisha na wanakiri kuwa walikosea kuwasilisha maombi yao ya msamaha, watasikilizwa, kupimwa na uamuzi utatolewa.
“Tunafanya hivyo kwa waliotusaliti na kutukosea na tunafanya kwa wale waliokwenda vyama vingine na kurudi. Hatuwanunui maana wanakuja wenyewe,” amesema.