Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimepewa wito wa kutumia vyema uhuru waliopewa hasa wa kufanya maandamano ya kistaarabu kinyume chake isitokee wakalalamika pindi maandamano hayo yakizuiwa
Ushauri huo umetolewa na Mfanyabiashara maarufu nchini Azim Dewji wakati akizungumza na wanahabari Februari 23.2024 ambapo amesema amelazimika kutoa rai hiyo kufuatia sintofahamu iliyotokea hivi karibuni Mbeya pale waandamanaji wa CHADEMA walipozuia msafara wa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Dotto Mashaka Biteko aliyekuwa kwenye ziara ya kikazi mkoani humo
Amesema mara zote uhuru wowote unakuwa na mipaka yake hivyo viongozi na wafuasi wa CHADEMA wanapaswa kutambua kuwa uhuru walionao sasa (wa kufanya maandamano hayo) unaweza kuzuiliwa kama mamlaka zitaona kuna mambo yanafanyika kinyume na matarajio ya utu, ustaarabu na uungwana wanaopaswa kuufanya
Aidha, Dewji ambaye ni mzaliwa wa mkoa wa Singida ameshauri Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA Tanzania Bara Tundu Lissu kuomba msamaha kutokana na tukio alilolifanya la kuwaongoza waandamanaji kuzuia msafara huo jambo ambalo halikubaliki kwa kuwa si la kiungwana
Amesema mara kadhaa amekuwa akiwasiliana na Lissu (kama mwana Singida mwenzake) na kumshauri mambo kadha wa kadha kwa kuwa mwanasiasa huyo amekuwa akitoa kauli zisizofaa dhidi ya viongozi wa serikali
Katika hatua nyingine Dewji amesema yeye ni miongoni mwa wadau wanaotamani kuona vyama vya upinzani vikiimarika kwa kuwa uimara wa CCM unategemea uwepo wa vyama vya upinzani imara vyenye kujenga hoja kinzani.