Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Askari kuongezwa Dar uchaguzi Serikali za mitaa

85501 Pic+uchaguzi Askari kuongezwa Dar uchaguzi Serikali za mitaa

Sat, 23 Nov 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es salaam. Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam limesema litaongeza askari 1000 kwa ajili ya kuimarisha ulinzi katika uchaguzi wa Serikali za mitaa utakaofanyika Jumapili Novemba 24, 2019.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Ijumaa Novemba 22, 2019 Kamanda wa kanda hiyo, Lazaro Mambosasa amesema askari hao wataimarisha ulinzi katika vituo vya kupiga kura, ofisi za Serikali na vyama vya siasa.

"Tumejiandaa vizuri kuhakikisha ulinzi na usalama unaimarishwa. Tunaongeza askari 1000 kutoka vikosi mbalimbali vikiwemo vya bandari na reli,” amesema Mambosasa.

Ameongeza, “tutatumia wadau wote ndani ya kanda, tutakuwa kila sehemu kwa kuwa maeneo unapofanyika uchaguzi kuwa machache, sehemu wahusika walikopita bila kupingwa wanakuwa salama pamoja na mali zao.”

Amebainisha kuwa kuna taarifa ya hujuma katika baadhi ya maeneo yenye ofisi za Serikali na vyama vya siasa, kwamba kuna waliopanga kuharibu mali na kufanya hujuma.

"Vipo viashiria mbalimbali vilivyojitokeza ikiwemo jaribio la kuchoma ofisi za serikali za mitaa, zipo taratibu ambazo mtu anaweza kufuata kama hajaridhika na sio kuharibu mali na kufanya vitendo vya uvunjifu wa amani,” amesema Mambosasa.

Chanzo: mwananchi.co.tz