Hai. Mbunge wa kuteuliwa Anne Kilango Malecela, amewataka wakazi wa kata ya Uroki wilayani Hai mkoani Kilimanjaro kumchagua mgombea wa CCM, Robson Kimaro kwa maelezo kuwa atasimama na kutatua changamoto zinazowakabili.
Kilango amesema CCM ikishinda itapambana kuhakikisha wananchi wa kata hiyo wanafikishiwa maendeleo.
Kilango ameyasema hayo leo Jumamosi Septemba 15, 2018 katika mkutano wa kufunga kampeni uliofanyika kijiji cha Uraa.
"Mimi ni mbunge ambaye nimeolewa na Mzee Malecela (John) waziri mkuu mstaafu, nitatumia nafasi yangu na ya mume wangu kumsaidia Robson Kimaro (mgombea wa CCM) kwa sababu hana haja ya kumtumia Freeman Mbowe, ananitumia mimi (Anne) kuhakikisha changamoto zenu zinapatiwa ufumbuzi,"amesema Kilango.
Mbowe ni mwenyekiti wa Chadema, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni na mbunge wa Hai.
Katika mkutano huo, Kilango amesema Mkoa wa Kilimanjaro huonekana kama wa upinzani, kuwataka wananchi kuachana na dhana hiyo.
"Mkoa wa Kilimanjaro huonekana wa upinzani sasa ifike mahali tuseme imetosha na jimbo hili la Hai mbunge wake ni kaka mbowe, lakini na nyie huyu kaka toka 2005 hazeeki?,” amehoji.
Akizungumza katika kampeni hizo mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Patrick Boisafi amesema chama hicho kitasimama kuhakikisha kinashughulika na changamoto zote zinazowakabili wananchi wa kata hiyo endapo watamchagua mgombea wa chama hicho.