Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Aliyegombea urais kupitia ADC awapa neno wanawake

657a322643c11a63b1654bc022532c27 Aliyegombea urais kupitia ADC awapa neno wanawake

Mon, 9 Nov 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

ALIYEKUWA mgombea urais wa Tanzania kupitia chama cha ADC, Queen Sendiga, amewataka wanawake wasikubali kutumika kuvunja amani kwa kuwa tunu hiyo ikipotea wao na watoto huathirika zaidi.

Alitoa mwito kwa wanawake watumie nguvu zao kuhimiza wanaume kutokubali kuunga mkono au kushiriki harakati zenye mwelekeo wa kuhatarisha na kuvunja amani.

Alisema hayo jana alipozungumza na HabariLEO kuhusu umuhimu na nafasi ya wanawake kulinda amani ya Tanzania baada ya Uchaguzi Mkuu.

"Mwanamke ndiye mlezi wa familia; na yeye na watoto ndio waathirika wakubwa wa majanga ya kijamii yanayotokana na ukosefu wa amani, hivyo wanawake wote bila kujali tofauti zozote zikiwamo za kisiasa, tuungane kuhakikisha tunalinda amani na mshikamano katika jamii na taifa letu kwa kuwaelewesha zaidi waume zetu madhara ya kupoteza amani,"alisema Queen.

Katika uchaguzi huo Queen na Cecilia Mmanga wa Chama Cha Demokrasia Makini walikuwa wanawake pekee miongoni mwa wagombea 15 wa urais wa Tanzania.

"Kama ni mumeo, mwambie mume wangu, Mungu ametujalia familia hii na watoto; tusaidiane kuilea; tazama nchi nyingine zilizochezea amani namna watu wanavyoteseka na watoto, wanawake, wagonjwa, wazee na wenye ulemavu ndio wanateseka zaidi; tusikubali kushiriki kupoteza amani, bali tulee watoto wetu ambao ni zawadi ya Mungu kwetu."

Katika kura zilizopigwa Oktoba 28 mwaka huu wananchi walimchagua John Magufuli aendelee kuiongoza Tanzania kwa miaka mingine mitano.

Magufuli aliapishwa Novemba 5 mwaka huu kwenye Uwanja wa Jamuhuri jijini Dodoma.

Queen alisema kwa kutumia karama na nguvu za kipekee kama akina mama na walezi katika familia na jamii, wanawake wawahimize kwa mifano wanaume ili wasikubali kuunga mkono au kutumika kuvuruga amani nchini.

"Tusikubali kutumika kama daraja la kuvunja amani, bali tutumie nguvu zetu za kipekee kuwaeleza wanaume; tena kwa mifano halisi ya nchi nyingine madhara ya kuchezea amani ili wasiunge mkono wala kushiriki kwa sababu watasababisha mateso kwa wake na watoto wao eti kwa siasa za mihemuko."alisema.

Alisema ukosefu wa amani huathiri mambo mengi yakiwemo ya kijamii zikiwemo huduma za afya, elimu, miundombinu na huduma za kiroho.

"Ukosefu wa amani huathiri hata upatikanaji wa huduma za kijamiii kama afya, dawa na miundombinu maana hospitali zikikosa dawa, wanaoathirika siyo wanachama wa ADC, CCM, au chama kingine chochote pekee, bali watu wa vyama vyote wanaathirika na mateso hayo," alisema Queen.

Tangu mwanzo wa mchakato wa kugombea urais wa Tanzania, Queen amekuwa akihimiza kampeni na siasa za kistaarabu ili kudumisha amani.

Vyombo vya habari vinamtaja Queen kuwa ni mwanasiasa aliyeonesha ukomavu wa kisiasa kwa kutamka hadharani kumpongeza Magufuli kwa ushindi na akaahidi kumpa ushirikiano kwa faida ya Watanzania.

Chanzo: habarileo.co.tz