Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

ACT Wazalendo huo ndio ukomavu wa kisiasa

2c13fd4d3981cc620011b5e9770d3fb2 ACT Wazalendo huo ndio ukomavu wa kisiasa

Tue, 8 Dec 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

JUZI Kamati Kuu ya Chama cha ACT Wazalendo ilitoa tamko kwa umma kuwa imeridhia chama hicho kushiriki kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa visiwani humo.

Tayari ACT Wazalendo kimependekeza jina la aliyekuwa mgombea urais wa Zanzibar kupitia chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamadi katika nafasi ya Makamu wa Kwanza wa Rais katika serikali hiyo, ambapo Rais, Dk Husein Mwinyi ameridhia na leo atamuapisha kushika rasmi wadhifa huo.

Chama hicho pia kimesema kitapeleka majina ya madiwani, wawakilishi na wabunge waliopatikana katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 28 kwa ajili ya kuchukua nafasi zao tayari kwa kazi ya ujenzi wa taifa.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa ACT Wazalendo, Ado Shaibu, uamuzi huo unalenga kulinda matakwa ya kitaifa ya ujenzi wa amani visiwani humo.

Tunapongeza uamuzi wa busara wa chama hicho kushiriki katika kuunda serikali ya umoja wa kitaifa kwani una maanisha unaheshimu uamuzi wa kidemokrasia wa wananchi wa Zanzibar wa kumchagua Dk Mwinyi kuwa Rais wao wa awamu ya nane.

Tuna imani kuwa viongozi wa ACT Wazalendo watakaopata nafasi kwenye serikali ya umoja wa kitaifa watashirikiana vizuri na Rais Dk Mwinyi na viongozi wengine wa serikali katika kusukuma mbele maendeleo ya Zanzibar na wananchi wake.

Wananchi wa Zanzibar wana imani na matumaini makubwa na Rais Dk Mwinyi kuwa atawaongoza vyema katika harakati zao za kutafuta maisha bora na ndio maana wamemchagua kwa kura za kishindo, hivyo hatutarajii ajitokeze yeyote kutaka kumuhujumu asifikie ndoto hizo za wananchi.

Aidha, tuna imani kwa wakati wote amani itaendelea kutamalaki Zanzibar ili wananchi waweze kufanya shughuli zao za maendeleo bila hofu wala vitisho vya aina yoyote.

Tunawasihi wale wote walioteuliwa na Dk Mwinyi kuunda serikali wawe kutoka chama tawala CCM au vyama vya upinzania kufanyakazi kwa maelewano na kumsaidia Rais katika majukumu yake mazito ya kuwatumikia wananchi wa Zanzibar.

Siasa za chuki, uchochezi na kukomoana sasa zifikie tamati kwani hazina faida yotote zaidi ya kukwamisha maendeleo ya Zanzibar na wananchi wake.

Sasa ni wakati wa Wanzibari wote bila ya kujali tofauti zao za kisiasa kuungana na Rais Dk Mwinyi kuchapakazi kwa bidi na maarifa ikwa maslahi ya Zanzibar na wananchi wake na kuwapuuza wale wote wanaotaka kuona visiwa hivyo havina utulivu wa kisiasa huku maendeleo yakidumaa.

Chanzo: habarileo.co.tz