CHAMA cha ACT-Wazalendo kimeitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), iweke wazi orodha ya majina ya wagombea wa chama hicho wa ubunge na udiwani, ambao walikata rufaa kwenye tume hiyo.
Taarifa kwa umma iliyotolewa jana na Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu, ilieleza kuwa wanahitaji majina hayo yawekwe hadharani, kutokana na taarifa ya NEC kwa umma iliyotolewa juzi kuhusu matokeo ya rufaa zilizowasilishwa.
Kwa mujibu wa chama hicho, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Dk Wilson Mahera katika taarifa yake juzi alisema tume hiyo imekubali rufaa 15 za wagombea ubunge na kuwarejesha katika orodha ya wagombea na imekataa rufaa 15 za wagombea, ambao hawakuteuliwa na pia imekataa rufaa 25 za kupinga walioteuliwa.
“ACT-Wazalendo tunasema taarifa hiyo ya NEC haijitoshelezi, ina walakini na upungufu kwa sababu haikuweka bayana majina na hata majimbo ambayo rufaa hizo tayari imezifanyiwa kazi,” alisema Shaibu.
Alisema huu ni muda muafaka kwa NEC kufanya kazi kwa weledi na uwazi, kwa kuyaweka hadharani majina yote ya wagombea waliokata rufaa, na majimbo husika yajulikane mapema ili chama hicho kiendelee na shughuli za kampeni