Mwanza. Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe inaongoza kwa kuwa na kiwango cha juu cha maambukizi ya Malaria kati ya halmashauri nane za Mkoa wa Mwanza.
Akizungumza leo Alhamisi Agosti Mosi, 2019 katika mkutano wa wadau wa kuhamasisha matumizi ya chandarua, mkuu wa Wilaya Nyamagana, Dk Philis Nyimbi amesema halmashauri ya Ukerewe inaongoza kwa kuwa NA asilimia 51 ya maambukizi ya malaria ikifuatiwa na Misungwi asilimia 38 na Buchosa (34).
Halmashauri nyingine za Mkoa huo ambazo hata hivyo Dk Nyimbi hakutaja viwango vya maambukizi ni Ilemalea, Nyamagana, Sengerema, Kwimba na Magu.
"Lazima tuweke na kutekeleza mikakati ya pamoja kupunguza maambukizi na kumaliza malaria katika maeneo yetu,” amesema Dk Nyimbi aliyemwakilisha mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella.
Mwakilishi wa Mpango wa Taifa wa kudhibiti Malaria (NMCP), Mponeja Peter amesema kiwango cha maambukizi kwa mkoa wa Mwanza ni asilimia nane, asilimia moja zaidi ya kiwango cha kitaifa cha asilimia saba.
"Kitaifa Mkoa wa Kigoma ndio kinara kwa kuwa na asilimia 24 ya maambukizi,” amesema Peter.
Pia Soma
Ofisa Rasilimali Watu wa ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Deogratius Charles amewataka viongozi wa Serikali kuanzia ngazi ya mitaa, vijiji, kata, wilaya na mikoa kusimamia utekelezaji wa mpango wa Taifa wa kutokomeza ugonjwa huo.Ametaja miongoni mwa mipango hiyo ni pamoja na ugawaji wa chandarua kupitia mradi wa PSI unaolenga kutokomeza malaria ifikapo 2030.
Mkuu wa wilaya ya Ukerewe, Carmel Maghembe amewaeleza washiriki wa mkutano huo uliohudhuriwa na wakuu wa wilaya, watendaji, wataalam na wadau wa maendeleo kuwa wilaya yake inatekeleza kampeni kadhaa kukabiliana na malaria ikiwa ni pamoja na kufyeka vichaka, kutokomeza madimbwi.