Bukoba. Naibu Waziri Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Dk Mary Mwanjelwa amesema kaya zote masikini zilizolengwa kufikiwa nchini zitaingizwa kwenye Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (Tasaf) awamu ya tatu sehemu ya pili baada ya Serikali kuridhia.
Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Agosti 2, 2019 mjini Bukoba baada ya kupokea taarifa ya Tasaf Mkoa wa Kagera.
Dk Mwanjelwa amesema malipo kwa kaya masikini yataanza kutolewa Agosti 2019 baada ya taratibu kukamilika.
Amesema Serikali imeridhia mpango wa Tasaf uendelee na kuwa awamu inayokuja ina maboresho mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwatambua walengwa kwa njia ya kielektroniki ili kuepuka kaya hewa.
Pia, amesema awamu inayofuata kaya masikini zenye watu wenye uwezo wa kufanya kazi watatakiwa kufanya kazi za kuwaingizia ujira na kuwa mfumo ulioboreshwa utatatua changamoto zilizokuwepo likiwemo suala la kaya hewa.
Naibu Waziri huyo amesema mpango wa kunusuru kaya masikini umesaidia familia nyingi kupiga hatua na kuwa mabadiliko makubwa yanatarajiwa katika awamu ijayo.
Pia Soma
- Mwanaharakati jela Uganda miezi 18 kwa kumtusi Museveni
- Katy Perry kulipa fidia ya Sh6 bilioni kwa kunakili wimbo
- Waziri Ummy azindua huduma ya dharura kwa wagonjwa mahututi