Dar es Salaam. Waziri wa Afya nchini Tanzania, Ummy Mwalimu amewaomba wasanii kutumia sanaa kuhamasisha watu kujua afya zao kwa kupima virusi vya Ukimwi.
Akifungua semina elekezi ya VVU kwa wasanii, Dar es Salaam nchini Tanzania, leo Jumatatu Novemba 11, 2019 Waziri Ummy amesema kundi hilo lina uwezo mkubwa wa kuisaidia Serikali katika mapambano dhidi ya ugonjwa huo.
“Mapambano dhidi ya Ukimwi si ya serikali pekee, nyie mna nafasi kubwa kupitia kazi zenu na mashabiki wanaowafuata huko kwenye mitandao ya kijamii.”
“Wala sitaki mtu atunge wimbo au filamu mie naomba kwenye hizo kazi zenu chomekeeni ujumbe wa kuhamasisha vijana wenzenu wakapime, wajitambue ili waanze kutumia dawa,” amesema Waziri Ummy
Amesema mtu aliyeathirika na kuanza kutumia dawa anajiondoa kwenye hatari ya kuambukiza wengine hivyo ni muhimu kuwa na idadi kubwa ya watu wanaojitambua.
Ummy amesema Serikali ilijiwekea lengo kufikia Desemba 2020 asilimia 90 ya Watanzania wawe wamepima kutambua hali zao lakini hadi sasa ni asilimia 62 pekee ndio wamefanya hivyo. “Tunaona muda unakwenda na lengo hilo hatujalitimiza ndio maana nimekuja kwenu leo nawaangukia wasanii mtusaidie kusambaza ujumbe na kuelimisha jamii, watu wapime,” amesema