Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Shirika la kimataifa linaloshughuka na masuala ya Chanjo (GAVI), Colette Selman.
Mazungumzo hayo yamefanyika Makao Makuu ya shirika hilo Geneva, Uswisi wakati wa kikao cha 75 cha Shirika la Afya Duniani (WHO).
Waziri Ummy amelishukuru shirika hilo kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kutoa huduma ya chanjo za watoto chini ya umri wa miaka mitano.
Amesema chanjo hizo ambazo zinawakinga watoto chini ya umri wa miaka mitano dhidi ya magonjwa yanayoweza kuzuilika kwa chanjo na kuongeza kuwa Tanzania imejipanga kuwafikia watoto wote, ili kuwakinga na magonjwa hayo.
Katika kikao hicho Waziri Ummy ameishukuru pia GAVI kuiwezesha Tanzania kupata chanjo za UVIKO-19 zipatazo milioni 11.2, ambazo zimewezesha uchanjaji hadi sasa kufikia asilimia 15 kati ya asilimia 70 ya kundi lililolengwa.
Waziri Ummy ametaja changamoto ya kasi ndogo ya kuchanja ni kutokana na kuwepo kwa imani potofu kwa baadhi ya wananchi kuhusiana na chanjo ya UVIKO-19, pamoja na wananchi kupendelea kuchanjwa majumbani au maeneo wanayofanyia kazi, jambo ambalo ni gharama katika utekelezaji wake.
Kwa upande wake Collete amemshukuru Waziri Ummy kwa kumtembelea na kujadili jinsi ya kushirikiana katika kuimarisha huduma za chanjo Tanzania.