Dar es Salaam. Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto nchini Tanzania, imesema imechukua jukumu la kusimamia huduma za kisaikolojia kwa mtoto Anna Zambi.
Waziri wake, Ummy Mwalimu ameeleza nia hiyo leo kupitia ukurasa wake wa Instagram akiahidi pia serikali kusimamia masuala yote yanayohusu ustawi wa Anna.
Anna alipoteza wazazi wake wote wawili na wadogo zake baada ya gari walilokuwa wakisafiria kusombwa na maji wakiwa safarini kuelekea kwenye mahafali yake.
Ummy ameandika, “Pole nyingi kwa binti yetu Anna Zambi. Hili jambo ni kubwa mno kwa mtoto huyu. Inaumiza sana. Ninamuombea kwa Mungu ampe nguvu na moyo wa uvumilivu katika kipindi hiki kigumu.
Nasi wizara ya afya tukiwa na dhamana ya kusimamia ustawi na maendeleo ya watoto nchini, tunachukua jukumu la kuratibu na kusimamia psychosocial support ya mtoto huyu pamoja na masuala mengine yanayohusu ustawi wake.”