Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Waziri Gwajima: Wauguzi wanaokiuka maadili wachukuliwe hatua kali

F2fb54c310c9358883d42bce0d5e88b2 Waziri Gwajima: Wauguzi wanaokiuka maadili wachukuliwe hatua kali

Sun, 19 Sep 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima ameliagiza Baraza la Uuguzi na Ukunga kuwachukulia hatua wauguzi na wakunga wanaovunja sheria, maadili, miongozo na miiko ya taaluma yao bila kuwaonea.

Dk Gwajima alitoa agizo hilo jana wakati akizindua Baraza la Uuguzi na Ukunga Tanzania, tukio lililofanyika katika ukumbi wa kituo cha baraza hilo kilichopo Kibaha, mkoani Pwani.

“Nitoe rai kwa Baraza, msisite kuchukua hatua za kinidhamu kwa mujibu wa taratibu na sheria zinazowaongoza na kamwe msimuonee mtu,” alisema.

Alisema baraza lina wajibu mkubwa wa kuhakikisha linalinda, kuimarisha na kuhifadhi afya ya jamii, usalama na ustawi kupitia usimamizi na udhibiti wa shughuli za mafunzo ya uuguzi na ukunga, huku akiweka wazi kuwa karibu asilimia 60 ya watoa huduma za afya hapa nchini ni wauguzi na wakunga kulinganisha na kada nyingine.

Aliendelea kusema kuwa, bado taaluma hiyo ina changamoto hasa katika upande wa utoaji huduma kwa wananchi, hali inayosababisha kuwepo kwa malalamiko mengi kutoka kwa wananchi.

Dk Gwajima alitoa rai kwa baraza kutimiza majukumu yake kwa weledi bila ya hofu ya kuingiliwa katika maamuzi yake ili kuboresha sekta ya afya, hususan kwenye eneo la uuguzi na ukunga nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa huduma za Uuguzi na Ukunga wa wizara hiyo, Ziada Sellah alimpongeza Waziri Gwajima kwa kuteua Baraza makini la Uuguzi na Ukunga ambalo litakuwa chachu ya kuleta matokeo chanya kwenye usimamizi na utoaji wa huduma kwa wananchi kwa kufuata sheria na kanuni za uuguzi na ukunga nchini.

Ziada alipongeza Baraza lililomaliza muda wake kwa jitihada kubwa walizofanya katika kufanya maboresho ikiwemo kuanzisha mfumo wa kanzidata ambao umewezesha kuanza kutoa huduma kwa njia ya mtandao, kupata idadi ya wauguzi na wakunga kwa urahisi na kuweza kuwahakiki kama wamesajiliwa.

Chanzo: www.habarileo.co.tz