Wazee Mkoani Mtwara wameiomba Serikali kuliangalia kundi hilo katika suala zima la matibabu, kutokana wazee mara kwa mara wananyemelewa na magonjwa kulingana na umri wao..
Hayo yamesemwa leo katika Kikao cha wazee na uongozi wa Mkoa wa Mtwara kilichofanyika mkoani hapa.
Katibu wa Baraza la Wazee Mkoani hapa, Seifu Chilumba amesema wazee hao mara kwa mara wananyemelewa na magonjwa mbalimbali kulingana na umri wao, hivyo ni vema wakapatiwa huduma hiyo, ili kuwaondolea changamoto inayowakabili.
"Tulikuwa tunaomba hawa wazee wapewe kadi ya bima ya matibabu na waliokuwa wengi kwa sababu hawana bima ya wanaendelea kuumia na wengine tunawakosa, hiyo ni changamoto kwa wazee wetu hawa," amesema Chilumba.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Marco Gaguti amesema watahakikisha wazee hao wanapatiwa huduma hiyo ya matibabu, kwani ni haki yao ya msingi.