Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Watu 781 wafariki kwa Corona tangu 2019

56be7c0a9511d08bd1080c77fe815d42 Watu 781 wafariki kwa Corona tangu 2019

Wed, 26 Jan 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

WIZARA ya Afya imetangaza kuwa watu 781 wamefariki kwa ugonjwa wa Corona tangu ulipoingia nchini mwaka 2019 huku maambukizi yakifikia 33,000.

Hayo yamesemwa jana na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu wakati wa mapokezi ya dozi 800,000 za chanjo ya UVIKO-19 aina ya Sinopharm kutoka Serikali ya China yaliyofanyika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere Dar es Salaam.

Akizungumza mara baada ya kuzipokea chanjo hizo, Ummy Mwalimu aliwataka Watanzania kujitokeza kupata chanzo hizo na kueleza kuwa kiwango kikubwa cha waathirika wa Uviko-19 ni wasiochanja.

Waziri Ummy alieleza kuwa kati ya Septemba 2021 mpaka Januari 23, 2022 watu 76 wamefariki kutokana na ugonjwa wa Uviko-19 kati ya vifo hivyo 73 hawakuchanja. Amesema watu 3147 walilazwa 2990 kati ya hao sawa na asilimia 95 hawakuchanjwa.

Aidha, Waziri Ummy alifafanua kuwa wagonjwa waliokuwa mahututi katika vyumba vya uangalizi maalumu (ICU) Januari 23, 2022 walikuwa 31 kati yao 30 walikuwa hawajachanjwa.

Amesema takwimu zinaonesha mpaka kufikia Januari 25, Watanzania 1,922,019 sawa na asilimia 3.33 walipata chanjo licha ya kukiri kuwa hali hairidhishi katika baadhi ya maeneo nchini.

"Tangu tuanze kutoa chanjo dhidi ya UVIKO-19 hapa nchini hadi sasa tuna dozi 8,821,210 zikijumuisha Sinopharm, Janssen, Moderna na Pfizer ambazo zinatosha kuchanja jumla ya watanzania 5,082,380,” amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy aliishukuru Serikali ya China kwa msaada wa chanjo hizo za awamu ya pili ambapo awamu ya kwanza Tanzania ilipokea dozi 500,000 ambazo zilitumika kuchanja watu 250,000.

Awali akizungumza Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendeleza ushirikiano uliopo huku akidai kuwa asilimia 80 ya watu wa China wamechanja.

“Tunaendelea kuipongeza Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano wao, imani yetu chanjo zitatumika vyema kwa kuzingatia asilimia 80 ya Watu wa China wamechanjwa,” amesema Chen Mingjian

Naye Mkurugenzi wa Kinga Wizara ya Afya, Dk Beatrice Mutayoba amesema chanjo hizo zina uwezo wa kukaa miaka miwili bila kuharibika, hivyo aliwaondoa wasiwasi Watanzania juu matumizi ya chanjo yaliyoisha muda wake.

“JJ inakaa miezi mitano tunafanya utaratibu wa kuzigawa ndani ya muda mfupi tunakuwa tumezimaliza, chanjo za Sinopharm ni miaka miwili na Pfizer zinakaa miezi 8,” amesema Dk Mutayoba.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live