Dar es Salaam. Taasisi ya Saratani ya Ocean Road imepanga kuwachunguza virusi vya homa ya ini watu 1,000 ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya homa ya ini duniani.
Taasisi hiyo imetenga siku tano kuanzia jana Julai 27, 2019 hadi Julai 31, 2019, uchunguzi huo utafanyika bila malipo.
Hayo yameelezwa leo Jumapili Julai 28, 2019 na mkurugenzi wa Idara ya Kinga na Huduma za Saratani, Dk Crispin Kahesa.
"Kwa siku ambazo si za maadhimisho huwa tunatoza Sh10,000 kuchunguza, tumefanya bila malipo ili kwenda sambamba na kauli mbiu ya mwaka huu ya wekeza kwenye mapambano dhidi ya homa ya ini," amesema.
Dk Kahesa amesema kuanzia jana na leo tayari watu zaidi ya 150 wamejitokeza kuchunguzwa iwapo wana maambukizi ya virusi hivyo au la.
"Kwa upande wa watu wazima mwitikio umekuwa mkubwa kwa kundi la wanawake kuliko wanaume na kwa kundi la vijana uwiano umekuwa sawa huku ikielezwa kwamba wengi waliojitokeza ni wale waliozaliwa kuanzia 1990 na kuendelea," amesema.
Pia Soma
- Waziri Mkuu apokea msaada vifaa vya mamilioni kutoka NMB
- Vanessa Mdee akwepa kumzungumzia Jux
- Lugola amvua madaraka mkuu wa kikosi cha usalama barabarani Arusha
Amesema sambamba na utoaji huduma ya uchunguzi na chanjo ya homa ya ini inaendelea kutolewa katika taasisi ya Ocean Road huduma hiyo pia inatolewa kwa watumishi katika maeneo yao ya kazi ikiratibiwa na hospitali hiyo kwa maombi maalumu.