Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Watakaokwamisha chanjo ya Polio kukiona

Polio Poliooo Watakaokwamisha chanjo ya Polio kukiona

Wed, 23 Mar 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wakati zoezi la kampeni ya chanjo ya Polio likitarajiwa kuanza Mikoa ya Songwe, Mbeya, Njombe na Ruvuma, Mkuu wa Wilaya ya Ileje mkoani Songwe, Anna Gidarya amesema kiongozi atakayekwamisha kampeni hiyo kuchukuliwa hatua .

Gidarya ameyasema hayo Machi 22, 2022 wakati wa kikao cha Kamati ya Afya Wilaya kilichoketi kwa lengo la kujadili mikakati ya kuanza kwa kampeni hiyo inayotarajia kuanza Machi 24, 2022 na kukamilika Machi 27, 2022.

Gidarya amesema zaidi ya watoto 23,000 walio chini ya miaka 5 wilayani humo wanatarajia kupatiwa chanjo ya polio ili kujikinga na ugonjwa huo ambao umeripotiwa nchi jirani ya Malawi.

Gidarya amesema wilaya ya Ileje imepokea dozi ya chanjo 25,000 kwa ajili ya kuchanja ambapo kila kaya itapitiwa kwa lengo la kubaini watoto waliochini ya miaka mitano sambamba na kuendea kutoa elimu ngazi ya vijiji, misikiti kanisani na kwenye minada.

“Wataalamu hakikisheni kila siku mnatoa takwimu za maendeleo ya zoezi la chanjo kutoka vituo 52 vilivyotegwa kwa ajili ya kutolea chanjo ili kukamilisha kampeni hii awamu ya kwanza kwa weledi.

“Wataalamu wa afya simamieni kampeni ya chanjo hiyo ili watoto waliolengwa wenye umri chini ya miaka mitano wanapata chanjo hiyo na mtumishi ambaye anaona hatahimili kwenye kampeni hii aache, kwani akibainika kukwamisha hatua kaliza kisheria zitachukuliwa dhidi yake,” amesema Gidarya.

Mganga mkuu wa Wilaya Ileje, Dk. Joyce Wilson Ongati amesema wamejipanga kufanya kampeni hiyo nyumba kwa nyumba na kwamba mpaka sasa wamefanikiwa kutoa elimu ngazi ya vibalozi, kitongoji na kijiji ambapo wanatarajia zoezi hilo kufanikiwa kwa asilimia 100.

“Wataalamu wa afya tutahakikisha tunashirikiana na viongozi wa serikali za vijiji, dini, mila na wananchi ili kufikisha taarifa sahihi kwa wazazi na walezi kuhusu chanjo ya polio,” amesema Dk. Joyce.

Upande wake Mratibu wa chanjo wilayani humo, Innocent Charles amesema mpaka sasa wamefanikiwa kutoa elimu kwa watoa huduma 55 ngazi ya jamii huku wataalamu 200 wakipewa elimu ya utoaji wa chanjo hiyo kwenye vituo 52 vilivyotegwa pamoja na kufika maeneo yasiyofikika kirahisi kwenye vituo hivyo.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live