WANAWAKE zaidi ya 100 nchini wamepatiwa matibabu ya awali ya saratani ya matiti kwa kuondolewa uvimbe kwenye matiti yao bila ya kulazimika kuyatoa kama ilivyokuwa ikifanyika hapo awali, matibabu yanayotolewa na Hospitali ya Saratani Ocean Road kwa kushirikiana na Hospitali ya Rufaa ya Taifa Muhimbili, tawi la Mloganzila.
Hayo yamebainishwa na Dk Julius Mwaiselaga , wakati akizungumza na Waandishi wa Habari jana wakati wa ufunguzi wa matukio mbalimbali yanayoendana na kukabiliana na saratani hiyo, hufanyika kila mwezi oktoba kuanzia tarehe moja hadi 30.
Alisema, kutokana na kuwezeshwa kwa huduma za tiba ya saratani kulikofanywa na serikali ya awamu ya tano, kwa sasa wagonjwa wenye saratani ya matiti hawalazimiki kukatwa matiti yao ili kutibu saratani isipokuwa uvimbe huo unaosababisha saratani unaweza kutolewa na titi likaendelea kubakia kama kawaida.