Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wanawake kunyonyesha miezi 6 mfululizo - Wizara

01f602a78d3ddcfa8dfad2d41ab26bec.png Wanawake kunyonyesha miezi 6 mfululizo - Wizara

Wed, 5 Aug 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MKURUGENZI Huduma za Lishe kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Grace Moshi amesema asilimia 58 pekee ya wanawake hufaulu kunyonyesha watoto wao maziwa yao pekee kwa kipindi cha miezi sita ya mwanzo baada ya kuzaliwa.

Alisema hayo juzi mjini hapa wakati wa warsha ya wanahabari kuhusu Wiki ya Unyonyeshaji Duniani iliyoanza kuadhimishwa Agosti Mosi na itafikia kilele Agosti 7 mwaka huu.

Alisema unyonyeshaji ni moja ya uwekezaji mzuri kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wachanga katika kuboresha afya na maendeleo ya jamii na mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Alisema katika kipindi cha miezi sita ya mwanzo mtoto anatakiwa kunyonya maziwa ya mama pekee. Alitaja baadhi ya sababu zinazofanya kinamama washindwe kutimiza wajibu huo ni pamoja na kazi nyingi zinazowakabili wanawake katika familia na jamii hivyo kukosa muda wa kupumzika na kunyonyesha watoto wao.

Pia mila na desturi na taratibu za jamii zinazohusu masuala ya ulishaji watoto, mojawapo ya taratibu hizo zinahusu kuwaanzishia watoto wachanga vyakula vya nyongeza mapema kabla hawajatimiza umri wa miezi sita unaopendekezwa na wataalamu wa afya.

“Kuna imani kuwa mtoto akilia mara kwa mara inamaanisha kuwa mama hana maziwa ya kutosha au mtoto ana kiu ya maji, wapo wanaoamini kuwa mama anapojifungua hana maziwa ya kutosha au maziwa yake ni mepesi, hizo ni baadhi ya imani potofu,” alisema.

Alisema mtoto anayezaliwa hupata maziwa ya kutosha kwa kipindi cha miezi sita ya mwanzo baada ya kuzaliwa na atahitaji kuanzishiwa vyakula vya nyongeza na maji ya kunywa pale anapotimiza umri wa miezi sita,” alisema.

Aidha alisema takwimu zinaonesha asilimia 97 ya watoto wenye umri wa miaka miwili wananyonyeshwa maziwa ya mama.

“Idadi ya watoto wanaolishwa chakula cha nyongeza ni asilimia 87 tu na watoto wa umri wa miezi sita hadi minane ndio wanaoweza kulishwa kwa usahihi,” alisema.

Alisema asilimia 30.3 ya watoto wa miezi sita hadi miaka miwili ndio wanaopewa chakula kwa usahihi, wanapewa milo inayotakiwa, mchanganyiko wa vyakula umekidhi makundi yote matano yanayotakiwa.

Kwa upande wake, Ofisa Lishe Valeria Millinga alisema baada ya miezi sita maziwa ya mama pekee hayatoshelezi mahitaji ya mtoto ya lishe na kuhitaji kulishwa taratibu vyakula mchanganyiko na vya kutosha ili akue vizuri.

Chanzo: habarileo.co.tz