Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wanaoishi na VVU wataja changamoto sita

Wed, 20 Jun 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dodoma. Mwenyekiti wa Baraza la Watu Wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (NACOPHA) Justine Mwinuka ametaja changamoto sita zinazowakumba watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (VVU).

Mwinuka ameyasema hayo leo Juni 19 2018 katika uzinduzi wa kampeni ya Furaha Yangu inayolenga kuhamasisha upimaji wa VVU kwa hiari hasa kwa wanaume na kuanza matumizi ya dawa za kufubaza makali ya ugonjwa wa Ukimwi (ARVs).

Mwinuka amesema iwapo changamoto hizo hazitafanyiwa kazi mipango mingi ya kuwasaidia wanaoishi na VVU haitafanikiwa.

Amezitaja changamoto hizo kuwa ni umbali wa vituo vya afya, upatikanaji hafifu wa dawa za kutibu magonjwa nyemelevu na wanaoishi na VVU kutumia muda mwingi katika kupata huduma za afya katika vituo vya kutolea huduma hasa katika maeneo yenye maambukizi makubwa.

“Changamoto nyingine ni lugha na unyanyapaa katika baadhi ya vituo vya kutolea huduma, kuchelewa kupata huduma za matibabu. Zisipotatuliwa zitarudisha nyuma lengo kubwa la kampeni hii,”amesema.

Kampeni hiyo imezinduliwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa na inashirikisha taasisi za kiserikali, za kimataifa na zisizo za kiserikali.

Wakazi wa Dodoma walijitokeza mapema asubuhi kwa ajili ya kushiriki katika uzinduzi wa kampeni hizo na baadhi walipata nafasi ya kupima VVU kwa hiari ndani ya Viwanja vya Jamhuri.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz