Serikali nchini inakamilisha mpango wa kuhakikisha raia wote wanapata Bima ya Afya bila kujali hali zao za kifedha. Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Afya Edward Mbwanga amesema mpango huo utawawezesha wanaoishi katika mstari wa umasikini wanapata huduma za mfumo wa Bima ya kitaifa.
“Serikali inayowajibika itawahakikishia raia wake bila kujali vipato vyao wanapata huduma bora za afya”amesema Mbwanga. Ameongeza “Changamoto ni kuchukua wale ambao hawakuwa na uwezo wa kulipia huduma hiyo. Ninafurahi kusema tunakamilisha mchakato huo”.
Akizungumza wakati wa mkutano wa wahariri wa NHIF mjini Dodoma, Mbwanga amesema kati ya Watanzania milioni 60, ni milioni 4.4 tu ndio wanachama wa mfuko wa Bima ya Afya.