Wananchi wa kata ya Igalla wilayani Ukerewe wameshauriwa kukitumia ipasavyo kituo cha afya Igalla pindi kitakapo kamilika na kuacha tabia ya kukimbilia kwenye tiba za kienyeji.
Akizungumza mara baada kuhakiki mradi wa ujenzi wa kituo hicho Mjumbe wa Kamati ya Siasa Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Mwanza Mohammed Lukonge ameeleza kuwa wananchi,wanapaswa kutumia kituo hicho kupata ushauri na huduma mbalimbali ikiwemo elimu ya afya ya uzazi wa mpango.
Ameeleza kuwa Serikali ya awamu ya sita imesogeza huduma ya afya kwa wananchi na ndio sera ya Chama Cha Mapinduzi hivyo waende kupata tiba zenye uhakika huku akijitolea mifuko miwili ya saruji kutekeleza mradi huo.
"Serikali inaendelea kutoa elimu ya afya ya uzazi kupitia wataalamu wa afya wa maeneo husika na tuna wahudumu katika maeneo mbalimbali ikiwemo vijijini wanaendelea kutoa elimu na tiba mbalimbali"anaeleza Lukonge.
Naye Mtendaji wa kata ya Igalla Sospeter Babis ameeleza kuwa mradi wa kituo hicho cha afya unatarajia kukamilika Mei 30 mwaka huu na kuanza kutoa huduma kwa jamii huku miundombinu inayojengwa ni jengo la wagonjwa wa nje(OPD),maabara,wodi ya wanaume na wanawake ,jengo la upasuaji na la kuhifadhia maiti