Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wakazi Dar wapewa mbinu za kujikinga Dengue, kupima bure

56781 Pic+dengue

Mon, 13 May 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Wakazi wa jiji la Dar es Salaam wametakiwa kuongeza kasi ya kufanya usafi wa mazingira na kuondoa mazalia ya mbu ili kupunguza uwezekano wa kuhifadhi mbu wenye vimelea vya Dengue.

Aidha, wametakiwa kuwahi hospitali na kwenye vituo vya afya pale wanapohisi mabadiliko kwenye miili yao ili wafanyiwe uchunguzi wa kitabibu kwani katika hospitali za Serikali kipimo cha Dengue ni bure.

Wito huo umetolewa leo Jumamosi Mei 11 na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Dk Yudas Ndungile wakati akihojiwa na kituo cha radio cha Clouds Fm.

Dk Ndungile amesema kasi ya kusambaa kwa ugonjwa huo imekuwa kubwa katika jiji hilo hasa wilaya za Ilala, Ubungo na Kinondoni.

Amesema hadi sasa takwimu zinaonyesha watu wasiopungua 1,000 wameugua ugonjwa huo katika jiji la Dar es Salaam tangu ulipotokea mlipuko Januari 2019.

“Jambo la muhimu ni kusafisha mazingira, nasisitiza kinga ni bora kuliko tiba tuondoe mazalia ya mbu katika maeneo yanayotuzunguka na zile sehemu tunapenda kukaa.”

Habari zinazohusiana na hii

“Kwa hiyo hata kama ni baa basi mmiliki ahakikishe mazingira ni masafi na hakuna mazalia ya mbu hivyo hivyo kwa maeneo mengine ya biashara, shule hata ofisi,” amesema na kuongeza:

“Kingine ni kuvaa mavazi yatakayofunika mwili hasa kwenye mikono na miguu, hakuna ushahidi wa kisayansi unaoonyesha kwamba ukipaka mafuta ya nazi mbu wa Dengue hawatakufuata.”

Dk Ndungile pia amesisitiza watu kuwahi hospitali na kwenye vituo vya afya pale wanapohisi mabadiliko kwenye miili yao ili wafanyiwe uchunguzi wa kitabibu.

Kuhusu gharama za vipimo amesema katika hospitali za Serikali kipimo cha Dengue ni bure.

Chanzo: mwananchi.co.tz