Dar es Salaam. Waziri wa Afya nchini Tanzania, Ummy Mwalimu amesema watu 14 ambao ni Watanzania wamepimwa na kubainika kuwa na virusi vya corona.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Aprili 13, 2020 na Waziri Ummy imeeleza idadi ya watu walioambukizwa virusi hivyo imeongezeka kutoka watu 32 hadi kufika 46.
Waziri Ummy amesema kati ya wagonjwa hao 14, 13 wanatoka Dar es Salaam na mmoja yuko Arusha.
Amesema wagonjwa hao wanaendelea kupatiwa matibabu na wamewekwa chini ya uangalizi wa wataalamu wa afya.
Aidha wataalamu wa afya wanaendelea kuwatafuta watu walioshirikiana na wagonjwa hao ili kuwapima kuona kama wamepata maambukizo.
Waziri Ummy ameendelea kuwataka wananchi kuchukua tahadhari zote za kiafya ili kujikinga na maambukizo ya virusi hivyo vya corona.