Makumi ya maelfu ya watu walio na ugonjwa wa kisukari cha aina ya kwanza nchini Uingereza watapewa teknolojia mpya, inayoitwa kongosho bandia, kusaidia kudhibiti hali hiyo.
Mfumo huo hutumia sensa ya sukari chini ya ngozi ili kuhesabu kiasi cha insulini kinachotolewa kupitia pampu.
Baadaye mwezi huu, NHS itaanza kuwasiliana na watu wazima na watoto ambao wanaweza kufaidika na mfumo huo.
Lakini wakuu wa NHS walionya inaweza kuchukua miaka mitano kabla ya kila mtu anayestahiki kupata fursa ya kuwa nayo.
Hii ni kwa sababu ya changamoto za kupata vifaa vya kutosha, pamoja na hitaji la kuwafunza wafanyikazi zaidi jinsi ya kuvitumia.
Katika majaribio, teknolojia - inayojulikana kama mfumo wa mseto uliofungwa - iliboresha ubora wa maisha na kupunguza hatari ya matatizo ya muda mrefu ya afya.Na mwishoni mwa mwaka jana, Taasisi ya Kitaifa ya Afya na Ubora wa Utunzaji (Nice) ilisema NHS inapaswa kuanza kuitumia.
Takriban watu 300,000 nchini Uingereza wana kisukari cha aina 1, wakiwemo watoto wapatao 29,000.Inamaanisha kuwa kongosho yao inashindwa kutoa insulini, homoni muhimu ambayo husaidia kugeuza chakula kuwa nishati.