Dar es Salaam. Licha ya Tanzania kukadiriwa kuwa na wagonjwa wa kifafa milioni moja, takwimu zinaonyesha zaidi ya asilimia 75 ya wagonjwa hao hupelekwa kwa waganga wa kienyeji ikiaminika kuwa wana mapepo.
Hayo yamebainishwa leo Jumatatu Februari 10, 2020 katika maadhimisho ya siku ya kifafa duniani ambapo mkoani Dar es Salaam elimu juu ya ugonjwa huo imetolewa na hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) katika viwanja vya Bakhresa, Manzese.
Akizungumza katika maadhimisho hayo daktari bingwa wa ubongo, uti wa mgongo na mishipa ya fahamu, Mnacho Mohammed amesema jambo hilo hufanyika kutokana na jamii kukosa uelewa kuhusu ugonjwa huo jambo ambalo pia huleta unyanyapaa.
“Wagonjwa wa kifafa wako katika hatari ya kifo mara sita zaidi ukilinganisha na jamii yote kwa ujumla na wagonjwa wengi wa kifafa ni vijana walio na umri wa wastani wa miaka 15,” amesema Dk Mohammed.
Amesema duniani kote kuna zaidi wa ya wagonjwa wa kifafa milioni 60 huku Afrika ikiwa ni bara ambalo limeathirika zaidi ambapo watu 20 hadi 50 ni wagonjwa kati ya watu 1000.
Akitaja sababu zinazochangia kuwepo kwa ugonjwa huo, Okeng’o Kigocha ambaye pia ni daktari bingwa wa ubongo, uti wa mgongo na mishipa ya fahamu wa NMH amesema ugonjwa huo hutokana na shoti katika ubongo inayosababisha hitilafu au jeraha kwenye ubongo hivyo mtu huanguka, kukakamaa, kuzimia au kutozimia na wakati mwingine kutoa povu mdomoni.
Pia Soma
- DPP: Watuhumiwa kesi uhujumu uchumi lipeni madeni
- Serikali ya Tanzania yataifisha madini ya Sh42.2 bilioni
- VIDEO: Sumaye ataja sababu kurejea CCM
“Na mtu anapodondoka kwa kifafa inatakiwa apewe huduma ya kwanza kwa haraka ikiwemo kumlaza kwa kutumia ubavu wa kushoto ikiwa ni baada ya kumtoa au kumlegeza nguo zinazombana,” amesema Dk Kigocha.