Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wagonjwa 26 wapandikizwa figo Dodoma

Figoo (600 X 400) Wagonjwa 26 wapandikizwa figo Dodoma

Wed, 16 Feb 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma, imefanikiwa kupandikiza figo wagonjwa 26 kuanzia Machi 22, 2018 kutoka mikoa mbalimbali nchini na wote wanaendelea vizuri.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Figo, Dk. Anthony Gyunda kwenye kipindi kilichorushwa na TBC Taifa.

“Uharibifu wa Figo unasababishwa na taka sumu pamoja na magonjwa yote yanayoathiri mwili kama kisukari, shinikizo la damu na pamoja na magonjwa yanayoambukiza na yasiyoambukiza,” alisema Dk. Gyunda

“Kuna hatua tano za matibabu ukigundulika na ugonjwa wa figo ikiwepo hatua ya haraka ambayo ni uchujaji wa damu na hatua ya mwisho ni upandikizaji wa figo,” alisema Dk. Gyunda

Aidha, Dk. Gyunda alitoa ushauri kwa wananchi kuepuka matumizi ya ulaji wa nyama kwa wingi, utumiaji wa sukari, mafuta ya kula pamoja na unywaji wa pombe ili kuepuka magonjwa yasiyokuwa ya lazima ikiwemo ugonjwa wa figo.

“Epukeni matumizi holela ya dawa, nendeni mkapate vipimo na ushauri wa wataalamu kwakuwa matumizi ya dawa kiholela sio mazuri kiafya na hii hupelekea kuua mfumo wa Figo.”amesema Dk. Gyunda

Hivyo basi, Dk. Gyunda amewasihi wananchi kupata vipimo kila mara, angalau mara mbili kwa mwaka ili kujua Afya zao na kuepuka gharama za matibabu.

Dk. Gyunda alisema katika hospitali hiyo wanapokea wagonjwa mbalimbali kutoka Mikoa jirani ikiwemo Iringa, Singida, Manyara na Mikoa mengine.

Pia, aliishukuru Serikali kupitia wizara ya Afya kwa kuwawezesha upatikanaji wa watumishi wenye weledi pamoja na vifaa tiba.

Mmoja wa wagonjwa katika kitengo cha Figo ambaye ni kijana mwenye mwenye umri wa miaka 17, alisema anapata matibabu ya uchujaji wa Damu katika hospitali hiyo na anaendelea vizuri.

Kwa upande wake, mtaalamu wa magonjwa ya uti wa mgongo, Dk. Waziri Jimmy alisema sio lazima kila tatizo kufanyiwa upasuaji Magonjwa mengine yanaisha kwa kutumia dawa.

“Ili kujua tatizo mapema lazima kupata vipimo kwa kuwaona wataalamu kabla ugonjwa haujazidi hadi kupelekea kufanyiwa upasuaji.” amesema Dk. Jimmy.

Mara nyingi magonjwa yasiyoambukiza hayana dalili hivyo ni muhimu kujua Afya yako kabla ya tatizo kujitokeza, afadhali kutumia gharama za vipimo kuliko kutumia gharama za matibabu.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live