Pwani. Wadau wa masuala ya Afya nchini Tanzania wamejadili changamoto ya ugonjwa wa malaria na hali ilivyo sasa nchini humo huku Watanzania wakishauriwa kutumia vyandarua vyenye dawa kujikinga na maambuzi.
Wadau mbalimbali walikutana jana Jumapili Septemba 8, 2019 mkoani Pwani kujadili changamoto ya ugonjwa huo chini ya Shirika la Johns Hopkins Center for Communication kupitia mradi wa VestorWorks kwa ufadhili wa Shirika la Msaada la Marekani (USAID) kupitia mfuko wa Rais wa Marekani wa kudhibiti Malaria (PMI).
Akizungumza katika kongamano hilo, Mkurugenzi wa Mradi wa VectorWorks, Waziri Nyoni alisema sio kila chandarua kinafaa kujikinga na mbu waenezao malaria.
"Chandarua chenye dawa kina kinga madhubuti, vinasaidia kufukuza mbu, kuzuia mbu kung’ata na dawa iliyopo katika chandarua ina uwezo wa kuua mbu na havina madhara kwa mtumiaji," alisema.
Mradi huo unafanya kazi katika maeneo matatu nchini ikiwamo katika sera, utekelezaji na ugawaji wa vyandarua.
"Tulihakikisha vyandarua vinapatikana katika vituo vya afya na maeneo mengine, mradi utakapomalizika mwaka huu, tunaamini Serikali na taasisi zitaendeleza pale mradi ulipokomea katika harakati hizi,'' alisema
Pia Soma
- Beki wa Manchester United atibiwa na "daktari wa miujiza" China
- Watumishi Wizara ya Kilimo wafikishwa mahakamani kwa madai ya kupokea rushwa
- Ofisa forodha TRA mahakamani kwa kuomba rushwa ya Sh500,000
- Serikali ya Tanzania kubadilisha hadhi Pori Tengefu la Wembere
Msimamizi wa Kitengo cha Kupambana na Maralia(NMCP),Winfred Mwafongo alisema chandarua kinatakiwa kutumika kwa lengo la kujikinga na malaria na sio kwa matumizi mengine.
“Kitengo chetu kipo kwa ajili ya kutoa maelekezo na kuhamasisha matumizi sahihi ya namna ya kutumia vyandarua na endapo kitachanika basi tunawashauri washone vizuri na kuendelea kukitumia na si kubadilisha matumizi,” alisema Mwafongo.