Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

WHO yaunga mkono uanzishwaji mfuko wa pamoja wa bima ya afya

Thu, 27 Jun 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema linaunga mkono jitihada za Serikali ya Tanzania za kuanzisha Mfuko wa Pamoja wa Bima ya Afya.

WHO inaunga mkono juhudi hizo wakati Serikali ya Tanzania ikiwa kwenye mpango wa kuunganisha Mfuko wa Afya ya Jamii na Bima ya Afya ili kuwezesha wananchi wote kupata huduma bora za afya.

Akizungumza leo Jumatano Juni 26, 2019 Mtaalamu wa Uchumi wa WHO nchini Tanzania Maximilian Mapunda amesema jambo la msingi ni kila mtu kupata huduma bora za afya bila kujali uwezo wake kifedha.

Mapunda amesema malipo ya matibabu kabla ya kuugua yanamsaidia mtu kuhudumiwa bila kipingamizi jambo wanalotilia mkazo zaidi.

"WHO tunatilia mkazo utoaji wa huduma za afya kwa wote bila kuwepo kikwazo cha fedha kwa hiyo mfuko wa pamoja wa bima za afya ni jitihada tunazounga mkono," amesema Mapunda.

Awali, baadhi ya wajumbe wa mkutano wa  huduma za afya kwa wote 'Health Universal Coverage' wamesema sekta binafsi inao mchango mkubwa katika kuhudumia afya ya jamii hivyo haipaswi kuwekwa pembeni katika mikakati ya utoaji huduma hizo.

Pia Soma

Mapunda amesema kitakachowasaidia watu wote kupata huduma kwenye hospitali za umma na binafsi sio malipo ya fedha  ya moja kwa moja isipokuwa malipo kabla ya matibabu.

Chanzo: mwananchi.co.tz